SADAKA YENYE UTATA
News
Published on 10/03/2025

SADAKA ya Rais William Ruto Jumapili iliendelea kuchafua hewa baada ya maafisa wa polisi kupambana na vijana waliojaribu kuvamia kanisa ambako kiongozi wa taifa alitoa Sh20 milioni wiki jana kufadhili miradi.

Rais Ruto akiwa Kaunti ya Uasin Gishu aliwapuuzilia mbali vijana hao na watu wanaopinga matoleo yake makanisani huku akitoa Sh20 milioni za kufadhili ujenzi wa jengo jipya la Kanisa ya AIC Fellowship Annex, Eldoret.

Aliapa kwamba vijana hawatapanga kuhusu matoleo yake makanisani akiapa kuendelea kujenga nyumba ya Mungu.

“Mimi sitatishwa na watu wa mitandao, nitaendelea kujenga makanisa lakini sijasema wasipende, la mno ni kwamba sharti tujenge makanisa,” Dkt Ruto akaeleza.

Jana, zaidi ya vijana 10 walijeruhiwa kwenye makabiliano kati yao na polisi walipojaribu kuvamia Kanisa la Jesus Fellowship Ministry wakitaka Sh20 milioni ambazo Rais Ruto alidaiwa kumpa kiongozi wa Kanisa hilo Askofu Edward Mwai Jumapili, Machi 2, 2025.

Vijana hao walipinga mchango huo wakisema ni kinyume na agizo lake (Rais Ruto) la kupiga marufuku maafisa wa serikali kutoa michango ya fedha makanisani.

Rais alitoa agizo hilo, baada vijana kufanya maandamano ya kuipinga serikali mwaka jana, kama njia ya kuzuia ufisadi na ubadhirifu wa rasilimali za umma.

Jana asubuhi Gen Zs walikongamana katika eneo la Roysambu, tayari kuandamana hadi katika Kanisa la Jesus Winner Chapel lakini wakazuiliwa na polisi waliowatawanya kwa kuwarushia vitoza machozi.

 

Aidha, vijana ambao walifaulu kuingia ndani ya Kanisa hilo, lililoko katika barabara ya Thika Mall Drive, kabla ya saa tatu za asubuhi, walinaswa na polisi waliokuwa wamevalia mavazi ya kiraia wakijifanya kuwa waumini.

Comments
Comment sent successfully!

Chat Online